Jumatatu , 25th Sep , 2017

Mtu mmoja amefariki na wengine zaidi ya 60 kunusurika kifo katika ajali ya basi la kampuni ya Allys Sports kupinduka katika barabara kuu ya Shinyanga kwenda Mkoani Mwanza.

Hayo amethibitisha, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga Kamishna Msaidizi wa Polisi, Simon Haule na kusema chanzo cha ajali hiyo ni mwendokasi ambao ulipelekea basi hilo kupoteza mwelekeo na kusababisha ajali ya hiyo.

"Majeruhi wengi wa ajali hiyo wamepelekwa katika hospitali ya Kola ndoto iliyopo Mwadui na wengine wamepelekwa katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa shinyanga kwa ajili ya kupatiwa matibabu. Dereva wa gari hilo amekimbia mara ilipotokea ajali", amesema Kamanda Haule.

 Kwa upande mwingine, Jeshi la Polisi la mkoa wa Shinyanga limesema linaendelea kumsaka dereva aliyesababisha ajali hiyo na kutoroka ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yake.