Ijumaa , 21st Oct , 2016

Kenya, Malawi, Zambia na Afrika Kusini zimetajwa kuongoza katika nchi zilizo na miundombinu isiyo rafiki kwa waendesha baiskeli na waenda kwa miguu.

Baadhi ya barabara nchini Kenya.

Taarifa hizo zimo kwenye ripoti iliyotolewa na Shirika la Mazingira la Umoja wa Mataifa, UNEP, ikiangazia maendeleo ya miundombinu kwenye nchi 20 za kipato cha chini na kati barani Afrika, Asia na Amerika ya kusini.

Ripoti imeeleza kuwa nchini Malawi pekee, asilimia 66 ya ajali za barabarani zilikumba waenda kwa miguu na waendesha baiskeli huku Kenya ikifuatia na asilimia 61.

UNEP imetaka uwekezaji zaidi kwenye miundombinu hiyo iwapo dunia inataka kupunguza hewa chafuzi itokanayo na matumizi ya magari.

Imependekeza serikali kutenga angalau asilimia 20 ya bajeti zao kwa ajili ya miundombinu ya waenda kwa miguu na waendesha baiskeli ili kuokoa maisha na kupunguza hewa ya ukaa.